Skip to main content

Kwenye Bonde la Upendo

 



“Siwezi kufanya hivi tena. Siwezi kuwa na wewe bila kukuona kwa namna ninavyotaka mimi. Shauku ya wewe kuwa wangu inazidi maadili yangu, inazidi uwezo wangu wa matamanio. Siwezi tena kujifanya kama sioni jinsi gani nikiangalia macho yako na kujidanganya kwamba… chochote tulicho nacho… kinaenda kwa jinsi unavyotaka.”

“Sijui nifanye nini ili uhisi ninavyohisi mimi. Labda huwezi kuona hili, lakini angalau jaribu kunitaka kama ninavyokutaka mimi, tumegawana hisia zetu, matatizo yetu, miili yetu. Kwanini iwe vigumu kuukubali uhalisia wa mahusiano yetu?”

“Unanipenda?”



Swali hilo. Swali ambalo hutaki kulisikia masikioni mwako. Swali ambalo huna jibu nalo. Kutarajia jibu kutoka kwa mtu usiyemtaka kumpoteza ni kama kisu kichanjacho moyoni. Ninajua hilo, kujua kwamba jibu litakalotoka litauma hata kama watabaki au kuondoka. Unatazama macho yake yaliyojaa hasira, ukihisi njaa iliyoko kwenye mtazamo wake. Maneno yanakukwama kooni na kushindwa kuongea. Unashusha macho, ukitamani aseme chochote ili kuvunja ukimya.

Anaangalia kando, na kuelekea mlangoni. Lakini anasita kabla ya kutoka chumbani. Unatamani kusema chochote kumbembeleza abaki, upande mwingine unatamani aende umruhusu awe huru na hisia zake ili pia kuulinda ukuta ulioujenga moyoni mwako.

“Siwezi kufanya hivi tena. Kwaheri.”

Anatoka akikuacha umesimama pale pale bila kujua cha kufanya. Mwili wako unapwaa baridi, mikono yako imejifunga kifuani kwa nguvu huku hisia za upweke zikipenya ndani yako na kukukamata kabisa. Unapumua polepole, macho yako yakielekeza mboni zake mlangoni, mlango ambao umeshuhudia akiufungua na kuondoka. Unajaribu kuelewa na kukubaliana na uhalisia wa upweke ulionao, lakini upweke huo inakuzidi nguvu na kujifanya ujikaze kwa kila nguvu uliyonayo.

Muda unasonga mbele, lakini bado umekwama palepale kwenye wakati ulioachwa na uhalisia mgeni. Huwezi kusonga mbele hata kama ukijitahidi kutumia nguvu zako zote. Wakati ambao neno lako moja lingebadili kila kitu hukulisema. Na sasa, majuto yanakutafuna kama njaa isiyoshiba. Maisha yako yamekuwa mzunguko usio na hisia, kuamka, kula, kufanya kazi na kulala, kama mashine ya kiotomatiki. Unajipa mawazo kuwa umefamya maamuzi sahihi, uamuzi uliotokana na kujilinda na kuhifadhi moyo wako. Lakini ule uchungu usiokomaa ndani ya kifua chako, unakusaliti, unakuwa sauti ya daima inayokukumbusha maamuzi yako.

Unachukua simu na kuanza kupitia mitandao ya ya kijamii, kidole gumba chako kinakosa nguvu, ukitafuta dalili yoyote ya wewe kuwepo kati ya misururu isiyoisha ya machapisho. Hakuna kitu kipya. Chapisho lake la mwisho ni picha yenu wawili, mikono yake ikiwa imezunguka kiuno chako, mkono wako ukiwa begani mwake, nyote wawili mkiwa kwenye tabasamu zito. Unakazia macho picha hiyo, ukikumbuka furaha uliyowahi kuihisi, ingawa uchungu bado upo ndani kabisa ya moyo yako, tabasamu laini linajitokeza bila hiari kwenye midomo yako.

Unazima simu yako na kutoka nje. Kumbukumbu ya jinsi mlivyokutana kwa mara ya kwanza inakurudia, siku zako za chuo kikuu., kozi tofauti mlizosoma watu mbali mbali mliokutana nao, na urafiki wa haraka lakini wenye kina mliouanzisha.



Uliwahi kuzungumzia ndoto zako kwa uwazi, ulilia kwa kicheko, ulikabiliana na maumivu kwa ujasiri. Lakini cha kushangaza, haujawahi kushawishika kuhusu uwezekano wa mapenzi. Kwako, mapenzi yalikuwa mtego, kujisalimisha kwa uhuru, gereza lililojengwa kwa petali za waridi na miiba. Maumivu ya zamani yalikuongoza kuapa kuwa hutamruhusu mtu yeyote adhibiti moyo wako tena.

Alijua. Alijua kuwa hutaki kwenda mbali zaidi kwenye mahusiano yenu. Lakini aliacha mapenzi yachukue nafsi yake kama mzizi laini ya maumivu matamu na machungu. Unakumbuka usiku ambao kila kitu kilibadilika baina yenu. Mchezo wa ukweli na kuthubutu ulisababisha busu mwanana lililozidisha matamanio ya mwili kati yenu. Busu hilo likazua muunganiko ambao usingeweza kupuuza. Kuta ulizojenga kulinda urafiki wenu zilibomoka chini ya uzito wa tamaa mliyoshiriki.

Hata hivyo, uliweka sheria mpya kwenye uhusiano wenu, ukauita urafiki wa kufaidiana. Bila ahadi wala matarajio ya uhusiano wa kimapenzi wa kudumu, bila hisia, miili tu ikijikunyata pamoja. Aliyakubali masharti yako, ingawa ulikuwa unaona upendo wake ukititrika usoni mwake, ila ulivaa upofu ukijifanya huoni chochote. Macho yake yalikaa juu yako muda wowote akuangaliapo, mguso wake ulikuwa mpole na alioyesha kutaka zaidi lakini aliogopa kuvuka mipaka ya masharti yako.

Sasa umekaa peke yako, mzigo wa maamuzi yako ukikuelemea. Unatazama taswira yako kwenye kioo. “Lazima niweke sheria nyingine,” unanong’ona. “Nitajutia baadaye.”

Unachukua simu yako na kuelekea nyumbani kwake. Moyo wako unadunda kwa nguvu kadri unavyokaribia mlango wake. Je, umechelewa? Huenda hisia zake zimefifia? Je, kama tayari amesonga mbele?

 Unasita kwa muda mchache na kisha kusukuma mlango kwa pupa, huwezi kuzuia hisia zako tena.

“Vera?” Sauti yake ni laini, yenye mshangao.

“Sielewi kinachonikuta,” unasema kwa haraka, ukizunguka ndani ya chumba. “Najihisi kama napoteza akili. Tumbo linavurugika, kichwa changu ni kama kimechanganyikiwa, umejaa wewe tu. Natamani nikutoe akilini mwangu lakini inashindikana.”

“Vera, kuna nini?”

“kuna nini kati yetu?” unauliza kwa sauti kali “Huwezi tu kuondoka kama unavyotaka unajua ni jinsi gani ninavyokuhitaji. Moyo unauma, Max. inauma kukupoteza.”

Chumba kinatulia. Unahisi joto likipanda mashavuni mwako baada ya mlipuko wako wa hisia, na kwa aibu, unageuza macho yako pembeni, ukizidiwa na hisia za aibu na majuto.

“Vera,” anakuita kwa sauti ya chini, “Unaingia kwenye upendo, sio ugonjwa wala sio jambo baya.”

“Ninakuchukia,” unakiri, machozi yakikutoka.

Anapiga magoti mbele yako, akishika mikono yako miwili. “Basi nichukie kwa kukupenda. Nichukie kwa kutaka zaidi kutoka kwako. Lakini usinisukume mbali na uwepo wako.”

“Max,”

Anatabasamu, “Kama itakufanya uhisi afadhali unaweza kusema ‘nakuchukia” kadri uwezavyo badala ya ‘nakupenda”

“Nakuchukia,” unanong’onoa kwa sauti ya chini ukitoa tabasamu la mbali.

“Inakusaidia?”

“Kidogo,” Unasema, ukimvuta karibu zaidi.



Busu lake ni la taratibu na lenye upole. Akikubusu, mikono yake anazungusha kiunoni mwako na kukuleta zaidi mwilini mwake bila kuacha nafasi yoyote baina yenu. Kadri akikubusu kuta ulizojenga kuzunguka moyo wako zinabomoka taratibu zikiacha hisia zako bila kinga. Safari hii, unafanya uamuzi wa makusudi kuziacha zianguke chini kabisa...

 


Comments